Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya
Juu (HESLB) imetoa siku 60 kuanzia tarehe 14 Machi, 2016 kwa wanufaika
wote wa mikopo wanaodaiwa na HESLB kujitokeza na kuanza kulipa madeni
yao kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.
Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi
Mtendaji wa Bodi ya Mikopo, Bw. Jerry Sabi imesema kuwa katika muda huu
wa siku 60 waajiri pia wanatakiwa kuhakikisha kuwa wanatekeleza wajibu
wao wa kisheria wa kuwasilisha taarifa za waajiriwa wao waliohitimu
katika vyuo vya elimu ya juu ndani na nje ya nchi.
Taarifa imesema kuwa inalenga
kuwakumbusha waajiri ambao bado hawatimizi wajibu wao kisheria (kifungu
cha 20) wa kuwasilisha majina ya waajiriwa wao wote ambao ni wahitimu wa
vyuo vikuu kwa HESLB ndani ya siku 28 tangu waajiriwe.
Adhabu ya kutotekeleza wajibu huu kwa
mwajiri ni faini ya shilingi milioni saba (Tshs milioni 7) au kifungo au
vyote kwa pamoja na kwa mnufaika wa mkopo atashindwa kutoa taarifa
hizo, adhabu yake ni kushitakiwa mahakamani.
Kwa mujibu wa sheria hiyo, baada ya
HESLB kupokea orodha kutoka kwa mwajiri, itafanya uchambuzi ili kubaini
wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu na kumwelekeza mwajiri kuingiza
makato ya marejesho kwenye mshahara wa mnufaika na kuwasilisha makato
hayo kwa HESLB.
Adhabu ya kutowasilisha makato kwa
HESLB ni faini ya asilimia 10 ya makato yote ambayo hayajawasilishwa na
faini hiyo inapaswa kulipwa na mwajiri.
Wajibu wa mnufaika wa mkopo na wazazi, walezi, wadhamini
Aidha, pamoja na wajibu wa mwajiri kama
ulivyofafanuliwa hapo juu, wanufaika wote wa mikopo ya elimu ya juu
tangu mwaka 1994, wana wajibu wa kisheria (Kifungu cha 19 cha sheria ya
HESLB), pamoja na mambo mengine, kuitaarifu HESLB kwa maandishi mahali
alipo na kuandaa utaratibu wa kulipa deni lake la mkopo wa elimu ya juu.
Aidha, HESLB inapenda kuwakumbusha
wazazi, walezi na wadhamini wa wanafunzi walionufaika na mikopo kuwa
wana wajibu wa kisheria (chini ya kifungu cha 22 cha sheria ya HESLB) wa
kuhakikisha kuwa taarifa muhimu za mnufaika waliyemdhamini zinaifikia
HESLB.
News Point inakusogezea habari kubwa za kila siku kutoka kila kona ya dunia. Ungana nasi kupitia Facebook, Twitter na Instagaram ili uwe wa kwanza kupata habari.
RELATED POSTS
BODI YA MIKOPO YATOA SIKU 60 KULIPWA MADENI YAO
Reviewed by Newspointtz
on
06:52:00
Rating: 5
0 comments:
Post a Comment