NEWSPOINTTZ.BLOGSPOT.COM

Ndanda Kosovo afariki Dunia Leo

    
 
Msanii wa muziki wa dansi Ndanda Kosovo amefariki dunia asubuhi ya leo katika hosptali ya taifa ya Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu.
     
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa mwanamuziki mwenzake Kardinal Gento, Ndanda alikuwa akisumbuliwa na matatizo ya vidonda vya tumbo, maradhi yaliyopelekea kulazwa katika hospitali ya Mwananyamala Dar es salaam.

Kardinali ambaye pia ni mjomba wake, amesema kuwa Ndanda alihamishiwa katika Hosptali ya Taifa Muhimbili siku mbili zilizopita kutoka Mwananyamala baada ya tatizo lake kushindikana kabla ya mauti kumkuta majira ya saa mbili asubuhi ya leo.

"Nilikuwa naye hospitali tangu jana, na nimekesha naye, ilipofika asubuhi hali yake ilikuwa nafuu, nikaondoka kurudi nyumbani kwa ajili ya chakula, nikaacha anafanyiwa mpango wa damu maana alikuwa amepungukiwa damu, lakini muda mfupi baada ya kuondoka hospitali hapo nikapigiwa simu kuwa Ndanda amefariki, ilikuwa mida ya saa 2 asubuhi” Amesema Gento.

Gento amesema taratibu za mazishi zinasubiri mama yake arudi Dar es salaam, ndipo wataamua kama asafirishwe au azikwe Dar es salaam.

“Mama yake alikuwa amekwenda Lubumbashi, lakini sasa inabidi ageuze na ndege, akisharudi ndiyo tutajua kama tunazika au tunasafirisha…… mama yake ni dada yangu, kwahiyo Ndanda ananiita mimi mjomba” Ameeleza kardinali Gento wakati akizungumza na EATV mapema leo asubuhi.

Ndanda Kosovo ni miongoni mwa waanzilishi wa band ya FM Academia katika miaka ya 90 lakini baadaye alihama na kuanzisha band ya Stono Musica akiwa na akina Maluu Stonch, Patcho Mwamba na wengineo.

Hadi mauti yanamkuta Ndada alikuwa akifanya shughuli za muziki kama msanii wa kujitegemea ‘Solo Artist’ akiwa na bendi yake ya Watoto wa Tembo huku akifanya shughuli za kibiashara
 
CHANZO EATV
Share on Google Plus

News Point inakusogezea habari kubwa za kila siku kutoka kila kona ya dunia. Ungana nasi kupitia Facebook , Twitter na Instagaram ili uwe wa kwanza kupata habari.

0 comments:

Post a Comment