NEWSPOINTTZ.BLOGSPOT.COM

Serikali yaandaa mpango wa ajira kwa vijana nchini



Serikali imeanzisha mpango maalumu wa mafunzo kwa wahitimu kutambua ujuzi katika sekta zisizo rasmi, ili kuwajengea vijana wigo mpana wa ajira kwa fani walizosomea.

Mpango huo unalenga kutoa mafunzo ya ufundi katika fani mbalimbali kwa vijana walioishia darasa la saba, kidato cha nne au sita na wanaohitimu vyuo mbalimbali.

Lengo ni kuwawezesha vijana kupata ajira na waajiri nao kupata watu wenye ujuzi wa kutosha.

Akizungumzia mpango huo juzi, Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Ajira Ofisi ya Waziri Mkuu, Robert Masingiri alisema changamoto kubwa kwa vijana ni ukosefu wa ajira hasa wanaomaliza shule bila kuwa na fani yoyote.

Masingiri alisema baada ya Serikali kuona upungufu huo, imeandaa mpango maalumu unaofadhiliwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) ili kutoa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi na wahitimu wa vyuo mbalimbali.

“Licha ya kutoa mafunzo hayo, tutatambua ujuzi uliopatikana kwa mfumo usio rasmi. Tutawapa wataalamu hao baada ya kukaa nao na kuona uwezo wao, hiyo itawasaidia kupata ajira hasa zinapokuja kampuni za uwekezaji au viwanda,” alisema.

Masingiri aliongeza kuwa nia ya Serikali ni kuongeza ujuzi kwa wafanyakazi ambao wako kazini, mpango huo utaanza na vijana 5,000.

Mkurugenzi wa ILO nchini, Mary Kawar alisema Tanzania imefanikiwa kuandaa mpango utakaosaidia vijana wengi kupata ajira 

“Kwa muda mrefu kumekuwa na pengo kati ya elimu ya darasani na utendaji. Naamini mafunzo haya yatatoa fursa ya pekee kuziba pengo hilo na kuongeza sifa za kuajiriwa,” alisema Kawar.

Mkurugenzi wa Taarifa za Soko la Ajira Ofisi ya Waziri Mkuu, Ahmed Makbel alisema mpango huo utakuwa na manufaa kwa waajiri na waajiriwa, kwa sababu wote watapata wanachohitaji.

Share on Google Plus

News Point inakusogezea habari kubwa za kila siku kutoka kila kona ya dunia. Ungana nasi kupitia Facebook , Twitter na Instagaram ili uwe wa kwanza kupata habari.

0 comments:

Post a Comment