NEWSPOINTTZ.BLOGSPOT.COM

KESI YA KAFULILA YAPIGWA DANADANA

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora imeahirisha kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi Jimbo la Kigoma Kusini iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, David Kafulila, kupitia chama cha NCCR-Mageuzi akipinga ushindi wa Mbunge Hasna Mwilima, wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kesi hiyo iliahirishwa jana na Jaji wa mahakama hiyo, Ferdinand Wambali, baada ya Wakili wa kujitegemea, Profesa Abdallah Safari, anamtetea mlalamikaji kuomba mahakama hiyo impatie saa 48 ili akamilishe hati za kiapo za mashahidi wake watano na baada ya hapo mahakama ipange tarehe nyingine ya kutajwa kwa ajili ya kuanza kusikiliza.

Jaji Wambali alikubaliana na ombi hilo na kusema hati za mashahidi zipelekwe kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora,  Shanmillah Sanwatt, zikiwa zimefungwa kwenye bahasha Machi 18, mwaka huu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kigoma.

Alisema siku hizi kuna utaratibu ulioanzishwa kwamba kila shahidi lazima awe na hati ya kiapo ndipo atoe ushahidi wake mahakamani.

Aidha, Jaji Wambali alisema hati za ushahidi zitakuwa zimefungwa na zitafunguliwa wakati wa shahidi anapoanza kutoa ushahidi wake.

“Nia ya mahakama ni kutatua migogoro na siyo kuongeza migogoro, hivyo jitahidini kuwasilisha hati za kiapo za mashahidi ili kesi hiyo isikilizwe na kutolewa uamuzi haraka,” alisema Jaji Wambali.

Alisema kutokana na matakwa ya kisheria, upande wa mlalamikaji unatakiwa kuwasilisha hati za kiapo za mashahidi zikiwa zimefungwa kwenye bahasha na zifikishwe hapo mahakamani mapema iwezekanavyo ili kesi hiyo imalizike haraka.

Jaji Wambali aliwataka mawakili wa pande zote kuhakikisha siku ya kesi kusiwapo na upande wowote kutofika hapo mahakamani.

Aidha, Jaji Wambali aliuhoji upande wa mshtakiwa unaoongozwa na Wakili wa Kujitegemea, Kennedy Fungamtama, kama una pingamizi dhidi ya maombi ya upande wa mlalamikaji.

Hata hivyo, upande huo ulidai kuwa hauna pingamizi dhidi ya maombi ya upande wa mlalamikaji na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa kwa ajili ya kuanza kusikiliza kesi hiyo.

Jaji Wambali alikubaliana na ombi hilo na kuahirisha kesi hiyo hadi Machi 29, mwaka huu kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kigoma.

Katika kesi hiyo, Kafulila atawakilishwa na Wakili Profesa Abdallah Safari pamoja na Tundu Lissu, wakisaidiana na Wakili wa Kujitegemea Daniel Rumenyela.

Kwa upande wa Mbunge Mwilima, atawakilishwa na Wakili wa Kujitegemea, Fungamtama pamoja na Mawakili wa Serikali wanaomwakilisha Msimamizi wa Uchaguzi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama washtakiwa katika kesi hiyo.

Katika kesi hiyo, Kafulila anaiomba Mahakama imtangaze kuwa mshindi kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi kifungu Na. 112(c) kwa madai kwamba yeye ndiye aliyepata kura nyingi kulingana na matokeo ya kila kituo kwenye fomu namba 21B na kwamba Msimamizi wa Uchaguzi alimtangaza Mwilima kinyume cha matokeo halisi.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kigoma jana ilifurika wanachama na viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa na watu wengine huku kukiwa na ulinzi mkali wa polisi waliokuwa na silaha za moto na mabomu ya kutoa machozi.

 

chanzo>mtembezi

Share on Google Plus

News Point inakusogezea habari kubwa za kila siku kutoka kila kona ya dunia. Ungana nasi kupitia Facebook , Twitter na Instagaram ili uwe wa kwanza kupata habari.

0 comments:

Post a Comment